Alhamisi, 31 Desemba 2015

Ukeketaji Mbulu


 
Helena Ringo: Mimi ni mfano wa watu waliokeketwa
Joan Michael: Nilipokeketwa damu na usaha ilitiriria
DK.Leonard Tlatlaa: Nimekutana na mtoto njia ya uzazi imefunga kwa ajili ya kukeketwa
Na  Lucy Ngowi
“NAKUMBUKA nilipokuwa na miaka mitano nilikeketwa. Kiukweli sitaisahau siku hiyo kutokana na maumivu niliyoyapata wakati wa kukeketwa na kuuguza kidonda.
“Wakati naugulia maumivu ya kukeketwa, nilikuwa nikiona katika sehemu zangu za siri damu na usaha vikitiririka, ila sijui mbele ya safari itakuwaje, kama atakuwa na uwezo wa kupata mtoto au la,” anasema Joan Michael (jina lisilo rasmi).
Binti huyo ambaye hivi sasa ana miaka 19 anazungumza kwa uchungu kuelezea mila potofu zinazofanywa na kabila lake la wabarbaig.
Anasema laiti kama angechelewa kukeketwa asingekubali tena kwani katika hali ya uhalisia ni ukatili uliopitilizwa, kwani hata kwenye maandiko matakatifu biblia hakuna mahali inapozungumzia kuhusu kumkeketa mwanamke bali kutahiri wanaume.
Anaiomba Serikali kuendelea kutoa elimu bila kuchoka kwa jamii hiyo ili kuwanusuru watoto wa kike ambao bado hawajakeketwa wasipatwe mateso ambayo alikabiliana nayo.
Si huyo tu, mfano wa binti  kama huyo ni mingi katika jamii za watu wanaokeketa ila wamekuwa wakiogopa kuzungumza hadharani kwa kuona aibu au kuhofia kutengwa na ndugu zake.
Kwa upande wake Mama Mchungaji wa Kanisa la Evangelistic Assemblies of God (EAGT), Odeliana Emmanuel anasema katika kijiji cha Qandach alikozaliwa, kata ya Endamila wilaya ya Mbulu, amekuwa akiona hali ya ukeketaji kwa watoto wa kike.
Anasema kama mama mchungaji na mwanaharakati wa kumtetea mtoto wa kike, amekuwa akizungumza na wale wanaowaandaa watoto kuwapeleka kwa ngariba, kuwaelimisha na kuwafundisha athari za kukeketwa kwa mtoto wa kike.
“Nimeelimisha ubaya wa ukeketaji. Kwa sasa umepungua lakini unaendelea kwa siri sana, hivyo wamebadili mbinu mpya ya kuwakeketa watoto kuanzia wanapoanza kutembea,” anasema mwanaharakati huyo.
Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Mbulu, Halmashauri ya Vijijini Justino Bayo anasema wilaya hiyo ina wenyeji wanaojulikana kama wairaqw, datoga au barbaig, nyisanzo na hadzabe.
Anasema suala la ukeketaji katika wilaya hiyo sasa hivi linapungua kwa wairaqw pamoja na wanyisanzo, lakini wa wabarbaig wanaendelea.
Lakini kama tendo hilo linafanyika katika mji  huo  ni kwa siri sana kutokana na kuogopa mkono wa sheria.
Bayo anasema chanzo cha hilo ni mila na desturi za wenyeji ambao wanaona kuwa mwanamke asipokeketwa ni kama najisi.
Naye Helena Ringo anaeleza kuwa, yuko miongoni mwa waliokeketwa, kwani mbaya zaidi alifanyiwa kitendo hicho akiwa na miaka 19 baada ya kumaliza chuo.
“Mimi ni mfano wa watu waliokeketwa. Nilikeketwa nikiwa nimemaliza chuo cha ualimu nikiwa na miaka 19,” anasema.
Mwanamke huyo ambaye fani yake ni mwalimu pia ni Mratibu wa Shirika linaloshughulikia ukeketaji wanawake na wasichana (AFNET), anasema mara nyingi mwisho wa mwaka wanawake wengi wanaandaa wasichana wao kwa ajili ya kukeketwa.
Hivyo kama mwanaharakati amekukwa akipita shule mbalimbali na kuwaasa wanafunzi wasikubali kukeketwa kipindi cha likizo.
Anasema amekuwa akipita katika shule za msingi na kutoa elimu hiyo, si hivyo tu bali mara nyingi pale anapokuta watu wamekusanyika huomba nafasi na kusema machache kuhusu ubaya wa ukeketaji.
“Nimekuwa nikiwaambia msipunguze kiungo chochote cha mtoto katika mwili wake, endapo mtafanya hivyo akimkamata mtu yeyote anampeleka mahakamani,” anasema mwanaharakati huyo.
Si hivyo tu, bali hata siku ya mtoto wa Afrika inayofanyika Machi 16, huwa anatoa elimu hiyo kuhusu ukeketaji.
Anakiri kuwa tatizo hilo ni kubwa, hivyo kama wataendelea kutoa elimu litapungua.
Anaongeza kuwa, baada ya kutolewa elimu mara kwa mara kuhusu athari za ukeketaji tatizo linapungua isipokuwa kwa watu wa vijijini ambao hufanya kimya  kimya ili wasijulikane wanachokifanya.
Ringo anasema chanzo cha ukeketaji ni imani iliyojengeka kuwa wanawake wanakeketwa ili kupunguza uhuni, lakini kiuhalisia ndio waliozidi kwa tabia hiyo mbaya.
Sababu nyingine ni kwamba wanamfanyia usafi msichana huyo kwa sababu sehemu hiyo inaficha uchafu.
Naye Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya Mbulu, Dk. Leonard Tlatlaa anasema hawajapata kesi za mtu aliyezidiwa kutokana na kukeketwa lakini kama daktari anaona kuna dalili zinazoonyesha bado kuna ukeketaji.
Na kwamba katika eneo hilo wanakeketa watoto katika umri mdogo kwa kuogopa mkono wa sheria.
“Kama daktari nimekutana na kesi ya mama wa mtoto kusema mtoto wake hana njia ya uzazi, nilipomcheki nikagundua njia iko wazi na kuna kidonda kilichotokana na kukeketwa,” anasema.
Anaongeza kuwa kati ya mwaka jana na mwaka huu amekutana na wagonjwa watatu wenye matatizo yaliyosababishwa na kukeketwa. Anasisitiza ukeketaji uliopo hivi sasa unafanywa katika umri mdogo.
Akizungumzia athari za ukeketaji ni kupoteza damu nyingi,  pale anapokeketwa mtu kinatokea kidonda na kutengeneza usaha ambao hupandisha homa na kuleta ufinyu wa njia ya uzazi hivyo mama wakati wa kujifungua huchanika.
Anasisitiza katika wilaya hiyo ukeketaji upo kila mahali.
Chanzo chake ni mila na desturi kwa kuwa watu hawataki kubadilika , pia wanasema kama msichana hajakeketwa hafai kuolewa. Hiyo ni dhama potofu.
Anasema pamoja na elimu inayotolewa jamii bado haijakubaliana na hiyo dhana ya kutokukeketa kutokana na mila na desturi. Hiyo ni kasumba yao bado haijawatoka.
Anashauri elimu iendelee kutolewa kuhusu athari zake baadaye kuhusu uzazi bora.
Pia hata mkono wa sheria unapokuwepo ufuate mkondo wake.
Mratibu wa Shirika la Afya na Maendeleo (Gesodea) pia Mwenyekiti wa Mtandao wa Malezi, Makuzi na Maendeleo ya mtoto mdogo, Tawi la Manyara  Jackson Suloo anakiri ukeketaji Mbulu umepungua kutokana na elimu inayoendelea kutolewa.
Pia anaamini miaka ijayo tatizo hilo litakuwa limekwisha, na kwamba tokea mwaka jana hadi sasa taasisi yake imezungumza na wazazi 83 kuhusu athari za ukeketaji.
Anaelezea chanzo cha ukeketaji ni kwamba ngariba wanatafuta kipato.
Kwa upande wake WP 4728 Koplo Glory kutoka kituo cha Polisi Mbulu anayeshughulikia dawati la jinsia anasema, kituoni hapo hakuna kesi zozote za ukeketaji zilizofikishwa.
Wilaya ya Mbulu ni mojawapo ya wilaya zilizopo katika Mkoa wa Manyara. Katika sensa ya mwaka 2012 idadi ya wakazi wa wilaya hiyo ilihesabiwa kuwa 320,279 waishio humo.
Mbulu imepakana na Mkoa wa Arusha pamoja na ziwa Eyasi upande wa kaskazini, wilaya ya Babati Vijijini upande wa mashariki, wilaya ya Hanang upande wa kusini na mkoa wa Singida kwa magharibi.
Wenyeji asilia ni Wairaqw  ama wanajulikana kama Wambulu. Makao makuu yapo Mbulu mjini na mji huu ulianzishwa wakati wa koloni ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani kwa jina la Neu-Trier.
Ukeketaji hapa nchini badi upo katika baadhi ya  maeneo kama mkoa wa Manyara, Dodoma, Arusha, Singida, Mara, Kilimanjaro na Morogoro.
Kati ya mikoa hiyo saba, Mkoa wa Manyara ndio unaongoza kwa asilimia 70.8 na Morogoro ndio wa mwisho kwa asilimia 21.1.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni