Alhamisi, 31 Desemba 2015

Ukatili wa Kijinsia Hanang



Daftari laandaliwa kudhibiti utelekezaji wa familia Hanang
  • Linawabana wanaume kutoa matumizi kwa watoto kwa kusaini
     
Na Lucy Ngowi
UKATILI wa kijinsia maana yake ni unyanyasaji wa aina yoyote anaokutana nao mwanaume au mwanamke kwa sababu tu ya jinsia yake.
Kwa mfano shambulio la mwili kama kumpiga mwanamke. Watu wengi kutokana na mfumo dume ulioko wanadhani kuwa kitendo hicho ni sawa kumbe sio.
Katika wilaya ya Hanang una ukatili wa aina nyingi ukiwemo wa kutelekeza mke, watoto ama vipigo kutokana na ulevi uliokithiri kwa wanaume.
Ofisa maendeleo ya Jamii wa Wilaya ya Hanang, Sabina Sulle anasema ukatili mkubwa wa kijinsia upo  kwenye utelekezaji wa watoto.
Anasema katika wilaya ya Hanang kesi za kutelekeza watoto zipo nyingi kwani wanaume wengi sana wanakwepa jukumu lao. Hivyo wanawake wanapozidiwa ndipo utafuta msaada kwao.
Anasema wanakutana na changamoto sana katika kutatua kesi za aina hiyo kwa kuwa wanaume wengi ni waongo, wanaahidi kuwahudumia baada ya kufikishwa kwao lakini, hawatekelezi.
Kutokana na hali hiyo imewabidi wawe na daftari ofisini ambapo mwanamme akikubali kuhudumia watoto wake kila mwisho wa mwezi anapeleka pesa hapo na kusaini, na mwanamke anakwenda kuchukua hapo hapo ofisini na kusaini, jambo ambalo limesaidia sana.
Anasema kesi kama hizo kwa mwaka huu zinazidi 30.
Kwa upande wake Mratibu wa Hanang Women Conceling and Development Association Mary Gitagno wa kata ya Ganana, anazungumzia ukatili wa aina nyingine ni kurithiwa baada ya mume kufariki.
“Ukatili mwingine ukifiwa unarithiwa. Kwanza unatakaswa. Wakati unaendelea kupata maumivu ya mume wako aliyefariki, anakuja mnyaturu analeweshwa pombe usiku, mwanamke unapewa sehemu ya kulala siku hiyo unajikuta uko mwenyewe, mnyaturu huyo anakuja kufanya tendo la ndoa na analipwa ukikubali unakuwa umeshatakaswa,” anasema Gitagno.
Anasema wanawake wengi hawapendi hali hiyo hukataa na kukimbia, ndio chanzo cha kupoteza mali za mume wake.
Anasema mambo mengi ya mila kama hayo hufanywa kisirisiri bila wengine kujua.
Mama mmoja Neema Alex (jina lisilo rasmi) mwenyeji wa Kata ya Basuti, tarafa ya Basuti, anasema mume wake alipofariki miaka mitano iliyopita, aliletewa mtu  kwa ajili ya kutakaswa.
Kwa maelezo ya  mama huyo, siku hiyo jambo ambalo sio la kawaida alijikuta akiwa amelala mwenyewe wanawake wenzake wakiwa hawako, usiku ulipokuwa mwingi, akaja mlevi mmoja na kutaka kumwingilia kwa nguvu, alishtuka na kukimbia.
Mtu Yule aliyeandaliwa alienda kudai ujira wake kwa waliomwagiza, huku nyuma yeye alikuwa akitafutwa ili apigwe lakini alikimbia na kwenda polisi.
Anasema kama jambo hilo lingefanikiwa angerithiwa na ndugu wa mume wake.
Anasema kwa kufanya hivyo ndio maana wanawake wengi wa vijijini wanaambukizwa magonjwa mbalimbali.
Daktari wa Kituo cha Afya cha Katesh, David Laizer anasema ndoa za utotoni zinazosababishwa na wazazi ni ukatili mkubwa, kwa kuwa kitendo hicho si kwa ridhaa ya muolewaji.
Pia anasema ukatili mwingine anaouana ni ule wa kuwapeleka watoto wa kiume shuleni na kuwaacha wa kike. Huo ni ukatili uliopitiliza kwa jamii hiyo.
Pia wanaume kutelekeza wake zao na watoto ni ukatili mkubwa kwa kuwa watoto wale wanateseka kwa kukosa mahitaji muhimu.
Wengi wanatelekezwa ama kuachika wanakuwa hawana sehemu za kwenda hali inayoleta mateso kwa watoto.
Kwa upande wake Mtendaji wa Katesh, Peter Mando anasema katika eneo hilo ukatili wa kijinsia upo sana kwa wanaume kuwapiga wake zao pamoja na kuwafukuza nyumbani.
“Migogoro kama hii tunaisuluhisha sana sisi na maofisa wa jamii, mahakama na polisi. Bado changamoto hiyo ni kubwa sana,” anasema.
Anasema katika kutatua migogoro hiyo wanawatumia maofisa wa maendeleo ya jamii kusuluhisha ikiwa ni pamoja na wazee wa mila na mahakama.
Chanzo cha jambo hili anasema ni mila na desturi za huko kwani wanaume wamekuwa wakiwabeza sana wanawake, ugumu wa maisha kwani wanandoa wengi wamekuwa wakizozana kwa ajili ya mahitaji ya nyumbani.
Si hivyo tu, bali na unywaji wa pombe pamoja na kutokufanya kazi, ndiyo inaleta shida hii.
Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Katesh A, Petro Tehhan anasema ukatili wa kijinsia eneo hilo unasababishwa  na mfumo dume pale baba anataka kusema kila kitu.
Pia kutokuelewana kwa mume na mke kunasababisha hali hiyo.
Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Hanang Kituo cha Katesh, Hamis Mwampelwa anazungumzia kesi za ukatili wa kijinsia zilizoripotiwa kituoni hapo ni 161, kati ya mwaka 2014 hadi sasa.
Anasema katika kesi hizo zile zilizofungwa ambazo hazikufikishwa mahakamani ni kesi 38, zilizofikishwa mahakamani ni 59 na zilizo chini ya upelelezi ni 70.
Kati ya kesi hizo, Mwampelwa anasema zilizopata mafanikio ni 15, ambazo hazikupata mafanikio ni 14, kesi iliyopo mahakamani kwa mwaka huu ni moja.
Anaeleza miongoni mwa kesi zilizoripotiwa za unyanyasaji wa kijinsia kuwa ni zile za kutelekeza familia, kubaka, shambulio la aibu pamoja na ukatili dhidi ya mtoto.
Anatoa mfano kwa kesi moja iliyofikishwa kituoni hapo siku za karibuni.
Kesi hiyo inamhusu mkazi wa Kitongoji cha Qedang’onyi Emanuel Lambo (50), aliyetarajiwa kufikishwa mahakamani baada ya kumtendea vitendo vya ukatili mtoto wake wa miaka tisa wa shule ya msingi kwa kumchoma na kisu chenye moto mkali maeneo mbalimbali ya mwili.
Mwampelwa anasema mtoto huyo alichomwa moto maeneo mbalimbali ya  mwili, kwenye kiwiko mkono wa kulia, kwenye shavu kushoto, shingoni kushoto, usoni na sehemu mbalimbali za mguu upande wa kulia kutokana na kulala kwa kaka yake, Mussa Emmanuel.
Anasema Oktoba 15 sueta la shule la mtoto huyo lilikuwa halijakauka, mama yake akamwagiza kaka yake akamuombee ruhusa shuleni, kisha mtoto huyo akalala kwa kaka yake huyo ndio ilikuwa chanzo cha baba kutenda ukatili huo.
Anasema mwanafunzi huyo aliwaambia wakati akitendewa ukatili huo, mama yake alijitahidi kumwokoa lakini baba yake alimkataza.
Tukio hilo la mwanafunzi kutendewa ukatili, lilijulikana baada ya mwalimu wake Bahati Mwiru kuhakiki wanafunzi shuleni na kugundua mtoto huyo hayuko, ndipo wenzake wakamwambia ana majeraha.
“Mwalimu aliendelea kuuliza wanafunzi hao majeraha  ni ya nini, ndipo wakamwabia amechomwa moto na kisu. Wakaijulisha kamati ya shule, mwenyekiti na mlinzi wakaenda kumchukua nyumbani,” anasema.
Anasema mwalimu huyo alitoa taarifa polisi baada ya mtoto huyo kukosekana shuleni kwa muda na alipouliza wenzake walimwambia anatibu majeraha aliyosababishwana baba yake, ndipo wakaanza kumfuatilia.
mwisho

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni