Alhamisi, 31 Desemba 2015

Nakala Ulemavu




Na Lucy Ngowi
ELIMU ya mahitaji maalumu hutolewa kwa watoto wenye matatizo ya kujifunza ili kuwawezesha kupata huduma za elimu.
Watoto hao ni wale walio na ulemavu wa kutokuona, viziwi, ulemavu wa akili, ulemavu wa usonji, viziwi wasioona, ulemavu wa viungo na walemavu wa ngozi.
Wenye mahitaji haya hutakiwa kupewa upendo wa hali ya juu kutoka kwa wazazi, familia, walezi, jamii inayowazunguka na wanafunzi wenzao shuleni ili nao wajione kuwa wanastahili kuwepo duniani.
Lakini kinyume cha hapo, huwaongezea maumivu na mateso watoto hao, kwani kwa kutokuwapa elimu stahiki hilo ni tatizo ama kwa kutokupewa huduma bora za chakula, malazi na mavazi.
Jamii inapotoa mapenzi ya kweli kwa watoto hawa hujisikia furaha sana. Sasa basi ni vema jamii kuzidisha mapenzi ya dhati kwa watoto hawa pamoja na serikali.
Mchango wa serikali nao unahitajika kwa kiasi kikubwa ili kuwafanya watoto hawa wasiwe wapweke. Inatakiwa serikali itoe huduma zote stahiki kwa watoto hawa ili waweze kusoma kwa bidii na hatimaye watakapomaliza wapate nafasi nzuri kikazi.
Kwa upande wake Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi inajitahidi kuwa na shule pamoja na vitengo mbalimbali kwa ajili ya watoto hao wenye mahitaji  maalum, lakini zimekuwa zikikabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo za fedha na vifaa maalum kwa ajili ya kufundishia.
Nimeanza kueleza hayo baada ya kupata nafasi ya kutembelea Shule ya Msingi ya Katesh A, iliyopo wilaya ya Hanang mkoa wa Manyara.
Shule hiyo pia ni ya bweni kwa ajili ya kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu ikiwemo wale wenye mahitaji maalum.
Katika shule hiyo ya Katesh A pia ni ya mchanganyiko kwa maana kwamba inachukua watoto wenye mahitaji maalum, mazingira magumu na watoto wa kawaida.
Wenye mahitaji maalum ni kama hao niliowaeleza hapo juu na waliotoka kwenye mazingira magumu ambayo wazazi wao wamekuwa wakihama hama na mifugo, kutokuelewana na maisha duni ya familia husika wapo 106.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Petro Tahhan anasema viziwi shuleni hapo wanasoma madarasa tofauti, wasioona wanachanganywa darasa la tatu  na wale wengine wasio na matatizo na wale wa mtindio wa ubongo hufundishwa na walimu maalum.
Anaelezea changamoto za wasioona kuwa wana upungufu wa vifaa vya kufundishia kama mashine za Braille. Mashine hizo zipo chache kwani ilitakiwa kila mwanafunzi asiyeona awe na yake.
Tahhan anasema wanafunzi hao wasioona wapo  nane, wavulana watano na wasichana watatu.
Darasa la awali yupo mmoja, la kwanza yupo mmoja, la pili wapo wawili, la tatu wapo wawili na la tano wapo wawili.
“Mashine nzima ni mbili walimu ambazo walimu wanatumia lakini kiuhalisia ilipaswa kila mwanafunzi awe na ya kwake. Kunatakiwa kuwe na walimu 15. Katika shule hii pia tuna walimu wasioona wawili ambao wanafundisha madarasa ya kawaida,” anasema mwalimu huyo.
Anasema wanafunzi hao wasioona hawana vitabu vya kuwafundishia kwa maana kuwa hawana vitabu vyao vinavyowahusu bali wanatumia vya kawaida.
Anasema miundombinu shuleni hapo sio rafiki kwani wanatakiwa kuwa na mazingira rafiki na vyoo vyao wenyewe.
Pia wana upungufu wa vifaa vya michezo, hata viwanja vyao vya kuchezea hakuna.
changamoto nyingine kwao ni suala la maji shuleni hapo ni tatizo, hivyo inabidi wazoee mazingira hayo, mara nyingine wanachota wenyewe ama wenzao wanawasaidia.
Na pia ulinzi ni shida shuleni hapo hakuna uzio.
Akizungumzia wanafunzi viziwi shuleni hapo  anasema wapo 27 ambao wanatakiwa kusoma miaka 10 badala ya saba ya kawaida. Darasa la kwanza, la tatu na la tano wanasoma miaka miwili miwili.
Wanasoma kwa mfumo huo kwa kuwa wanakuwa wanachelewa kuelewa kile mwalimu anachofundisha, ila madarasa mengine wanasoma mwaka mmoja mmoja.
Anasema shule hiyo ina upungufu wa vyumba vya madarasa hivyo wakati mwingine wanachanganywa wote katika chumba kimoja, pia wana tatizo la walimu wenye uwezo wa kufundisha watoto hao wenye mahitaji maalum.
Jambo lingine ni kwamba mihtasari wanayotumia ni ya kawaida haiendani na mahitaji yao.
Tatizo lingine ni kwamba hawana kamusi yao ya lugha ya alama.
Analitaja kundi lingine ni la albino ambao hivi sasa wapo nane, awali walikuwa 11 lakini watatu wamemaliza. Wanafunzi hao wanakabiliwa na tatizo la vifaa vya kujikingia ngozi yao kama mafuta yao na kofia.
Mwalimu mkuu huyo anasema wale wa utindio wa ubongo wapo watano, kati ya hao wawili ni wa kiume na watatu wasichana.
“Hawa wa utindio wa ubongo kwa sasa wapo nje ya shule. Wana upungufu wa walimu, mihtasari yao hakuna, hivyo kwa sasa wanapelekwa na wazazi wao shuleni hapo,” anasema mwalimu huyo na kuongeza kuwa kitengo hicho cha utindio wa ubongo kimeanza mwaka huu.
Kwa wanafunzi hao wa utindio wa ubongo, wanafundishwa na mwalimu wa kiume lakini walitakiwa walimu wa kike pia kwa sababu wanahitaji huduma za ziada kama kusaidiwa kwenda chooni ama kulishwa ama wakati mwingine kuvalishwa nguo kama wamejichafua.
Anasema kuwa shule hiyo haina mipaka wanaweza kwenda kutoka mikoa yote nchini, kwani mbali na wakutoka wilaya hiyo wengine wanatoka Tanga, Simanjiro, Singida, Babati na Mbulu.
Tahhan anashauri shule hiyo ingeangaliwa kwa jicho la kipekee kwa kuwa ni shule ya mahitaji maalum, kwani fedha wanazopewa ni kwa ajili ya chakula tu, hakuna ya kumlipa mlezi wala vinginevyo.
Kwa upande mwingine Mwalimu Mkuu msaidizi Caroline Lema anasema kama serikali imeamua kutenga shule hiyo hapo Hanang iwasaidie watoto kwa kuwapa vifaa vyao stahili ili ule umaalum uonekane.
“Watoto hawa inatakiwa watibiwe walau kwa mwaka mara mbili, kama ni wasioona inabidi wachunguzwe wote uoni wao lakini kwa pesa inayotolewa inatosheleza kwa chakula tu, sasa hii ni elimu maalum kwa vipi? kama hata hela ya matibabu hakuna?,” anahoji Lema.
Mwalimu huyo anasema kuna watoto watatu ambao wanatakiwa waende katika hospitali ya KCMC Kilimanjaro kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji haraka iwezekanavyo lakini kwa kuwa hakuna fedha hawajaenda.
Anasema kila halmashauri yenye elimu maalum huwa anakuwepo ofisa elimu maalum lakini anakuwa na fani moja labda ya viziwi sio utindio wa ubongo, lakini anafikiri ilibidi kuwe na maofisa mchanganyiko ama huyo ofisa asiwe amejikita kwenye eneo moja tu.
Kwa upande wake mwalimu Anna Mark anayefundisha wanafunzi wasioona shuleni hapo anasema changamoto kubwa ni ukosefu wa vifaa vya ufundishaji.
“Vifaa vingi tunaweza kuvitengeneza wenyewe ambavyo vinawasaidia watoto hawa,” anasema mwalimu huyo na kuongeza kuwa upungufu wa mashine za Braille ni changamoto kwake na wanafunzi hao.
Akiwaelezea watoto hao jinsi wanavyopokea kile anachowafundisha anasema wanajitahidi kupokea vizuri japo kwa taratibu sana.
Mwanafunzi wa darasa la pili Imani Agustine anasema anapata ugumu pale anapoandikiwa neno jipya hata kama amefundishwa anashindwa kulisoma.
Naye Paulo Marcelly anasema somo la hisabati linampa shida hivyo anaiomba serikali kuwapatia vitabu na mashine.
Naye Ofisa Elimu Maalum wa Hanang, Albart Machua anasema katika shule ya Katesh A kuna changamoto nyingi sana ikiwemo vyumba vya  madarasa na vifaa vya kufundisha na kujifunzia.
Anasema kuhusu fedha za matibabu za wanafunzi hao hutolewa na halmashauri, japo kuna baadhi ya wanafunzi walihitajika kwenda KCMC kufanyiwa upasuaji wa macho, hawakwenda kwa kukosa pesa.
Pia anaomba serikali ijitahidi kufikisha hela za ruzuku kwa wakati ili wanafunzi hao waweze kuhudumiwa.
Kwa upande wake Ofisa elimu wa wilaya ya Hanang, upande wa shule ya msingi, Gwandu Omari anasema wanafunzi hao wanatakiwa watengwe kutokana na ulemavu walionao.
“Katika shule ya Katesh A kuna changamoto ya mabweni yaliyopo hayatoshi, ni chakavu, magodoro machache, jiko na bwalo vyote vina upungufu,” anasema.
Pia anasema baadhi ya fani zinazohusu watoto wenye mahitaji hayo kuna upungufu wa walimu, wapo watano ila mahitaji ni 13.
Hata mashine za watoto wenye shida ya macho ni chakavu zinafanyiwa matengenezo kila wakati, karatasi zake ni za shida.
Viziwi wanatakiwa wawe na mashine na tochi za kuwakagua hali zao za masiko kila wakati lakini hakuna.
Albino nao ni shida huduma zao, wanahitaji kuchekiwa ngozi zao mara kwa mara. Kuna gharama za kila wakati kliniki na kupewa mafuta maalum.
“Hawa wa mtindio wa ubongo huduma zao ni za karibu sana popote anahitaji msaidizi, inapokuwa ni mwalimu peke yake kazi inakuwa kubwa,” anasema.
Akizungumzia miundombinu bado kuna tatizo  kubwa hakuna ufumbuzi wa haraka wa kuongeza madarasa na mabweni yaliyopo ni chakavu yanatakiwa kubomolewa.  
Kwa upande wake Mratibu wa Elimu Maalum kutoka wizara ya elimu, Gryson Mlanga anataja idadi za shule maalum na vitengo katika maeneo mbalimbali  nchini.
Mlanga anasema idadi za shule kwa wasioona zipo nne Tanzania nzima ambazo ni Irente Lushoto, Buigiri Chamwino, Malangali Sumbawanga na Furaha Tabora.
“Hizi ni shule maalum. Uoni hafifu na albino na wasioona kabisa,” anasema.
Kwa upande wa shule mchanganyiko zipo 34, ambapo katika shule hizo darasa la kwanza na la pili wanakuwa na madarasa maalum, kuanzia la tatu mpaka la saba wanachanganyika na wasiokuwa na ulemavu.
“Hizi shule zina mabweni. Nazo ni uhuru mchanganyiko iliyoko Dar es Salaam, Pongwe Tanga, Same Kilimanjaro, Mwereni Moshi, Longido, Katesh A wilayani Hanang, Ikungi Singida na Hombolo mkoani Dodoma,” anasema.
 Mratibu huyo anasema kwa viziwi shule maalum zipo 11 na vitengo 37. Vitengo ni vile vinakuwepo kwenye shule za kawaida ambapo hutengwa madarasa maalum.
Anataja baadhi ya shule hizo za viziwi kuwa ni Buguruni, Mwanga, Njombe, Tabora viziwi, Twivila Iringa na Tumaini Singida.
Baadhi ya vitengo kwa viziwi ni Mugeza huko Bukoba, Msasani Dar es Salaam, Maweni Kigamboni, Twiga eneo la Temeke na Basil Mramba huko Mwanga, Kilimanjaro.
Kwa upande wa ulemavu wa akili zipo shule tano maalum ambazo ni Sinza maalum, Mtoni Maalum, Miyuji Dodoma, Bethlehemu Ifakara na Lulindi huko Masasi.
Ina zaidi ya vitengo 250 ambavyo ni Leganga Arusha, Rutihinda Kinondoni, Umoja Kinondoni na Msasani zote zikiwa mkoa wa Dar es Salam.
Ulemavu mwingine ni ule wa usonji ambapo watu hao wameathirika katika mishipa ya fahamu, unaathiri mahusiano, ufahamu na mawasiliano.
Katika huo kuna vitengo vitano kwa Dar es Salaam na Morogoro. Vipo Msimbazi Mseto, Patandi na Uhuru Arusha, Kiwanja cha ndege Morogoro na Mbuyuni.
Wengine ni wanafunzi wasioona amboa wako kwenye vitengo. Uhuru mchanganyiko, Mwanga, Mugeza Bukoba, Makalala Mufindi na Katumba Two, Tukuyu.
Akizungumzia wenye mahitaji maalum ya ulemavu wa viungo husoma kwenye shule za kawaida kama hawana shida kubwa.
Hao wenye ulemavu wa viungo wengine huwepo Jesho la Wokovu jijini Dar es Salaam, Faraja mkoani Kilimanjaro, Malangali, Kabanga Kasulu mkoani Kigoma huko nako wapo wasioona na albino. Na Siuyu mkoani Singida.
Mratibu huyo anasema changamoto zipo na wanazipata kwenye taarifa mbalimbali zinazowafikia, pia wanapopata fursa za kutembelea shule hizo hukutana nazo.
Akielezea mahitaji wanayopaswa kupewa wanafunzi hawa kutoka serikalini ni chakula, malazi safi, matibabu, nauli wakati wa likizo, vifaa vya kufundishia na vya kujifunzia kulingana na mahitaji husika.
“Kama wizara tunatarajiwa watoto hawa wahudumiwe katika maeneo hayo,” anasema.
Kuhusu vifaa vya watoto hao, anasema kwa muda mrefu vilinunuliwa na wizara, lakini ikafika mahali ikaamuliwa vitolewe na halmashauri na sasa hivi kuna mradi unaotekelezwa nchi nzima wa kuvinunua.
“Zitanunuliwa mashine 800 za Braille, shime sikio 1000, fimbo nyeupe 1200 pia tunaendelea kuchapisha vitabu 8000 ambavyo vitasambazwa vya mtaala mpya,” anasema na kuongeza kuwa vifaa hivyo vitatolewa kabla ya mwaka huu haujaisha.
Anasema suala la walimu ni jukumu la Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Anasema mpango wa baadaye ni kwamba kila halmashauri iwenna shule moja maalum kwa ajili ya wanafunzi wa mahitaji maalum.
Anasema takwimu sahihi za wanafunzi hao hazipo ila kuanzia sasa zinaanza kukusanywa mpaka mwaka 2020 zitakuwa zipo tayari.
mwisho

Ukatili wa Kijinsia Hanang



Daftari laandaliwa kudhibiti utelekezaji wa familia Hanang
  • Linawabana wanaume kutoa matumizi kwa watoto kwa kusaini
     
Na Lucy Ngowi
UKATILI wa kijinsia maana yake ni unyanyasaji wa aina yoyote anaokutana nao mwanaume au mwanamke kwa sababu tu ya jinsia yake.
Kwa mfano shambulio la mwili kama kumpiga mwanamke. Watu wengi kutokana na mfumo dume ulioko wanadhani kuwa kitendo hicho ni sawa kumbe sio.
Katika wilaya ya Hanang una ukatili wa aina nyingi ukiwemo wa kutelekeza mke, watoto ama vipigo kutokana na ulevi uliokithiri kwa wanaume.
Ofisa maendeleo ya Jamii wa Wilaya ya Hanang, Sabina Sulle anasema ukatili mkubwa wa kijinsia upo  kwenye utelekezaji wa watoto.
Anasema katika wilaya ya Hanang kesi za kutelekeza watoto zipo nyingi kwani wanaume wengi sana wanakwepa jukumu lao. Hivyo wanawake wanapozidiwa ndipo utafuta msaada kwao.
Anasema wanakutana na changamoto sana katika kutatua kesi za aina hiyo kwa kuwa wanaume wengi ni waongo, wanaahidi kuwahudumia baada ya kufikishwa kwao lakini, hawatekelezi.
Kutokana na hali hiyo imewabidi wawe na daftari ofisini ambapo mwanamme akikubali kuhudumia watoto wake kila mwisho wa mwezi anapeleka pesa hapo na kusaini, na mwanamke anakwenda kuchukua hapo hapo ofisini na kusaini, jambo ambalo limesaidia sana.
Anasema kesi kama hizo kwa mwaka huu zinazidi 30.
Kwa upande wake Mratibu wa Hanang Women Conceling and Development Association Mary Gitagno wa kata ya Ganana, anazungumzia ukatili wa aina nyingine ni kurithiwa baada ya mume kufariki.
“Ukatili mwingine ukifiwa unarithiwa. Kwanza unatakaswa. Wakati unaendelea kupata maumivu ya mume wako aliyefariki, anakuja mnyaturu analeweshwa pombe usiku, mwanamke unapewa sehemu ya kulala siku hiyo unajikuta uko mwenyewe, mnyaturu huyo anakuja kufanya tendo la ndoa na analipwa ukikubali unakuwa umeshatakaswa,” anasema Gitagno.
Anasema wanawake wengi hawapendi hali hiyo hukataa na kukimbia, ndio chanzo cha kupoteza mali za mume wake.
Anasema mambo mengi ya mila kama hayo hufanywa kisirisiri bila wengine kujua.
Mama mmoja Neema Alex (jina lisilo rasmi) mwenyeji wa Kata ya Basuti, tarafa ya Basuti, anasema mume wake alipofariki miaka mitano iliyopita, aliletewa mtu  kwa ajili ya kutakaswa.
Kwa maelezo ya  mama huyo, siku hiyo jambo ambalo sio la kawaida alijikuta akiwa amelala mwenyewe wanawake wenzake wakiwa hawako, usiku ulipokuwa mwingi, akaja mlevi mmoja na kutaka kumwingilia kwa nguvu, alishtuka na kukimbia.
Mtu Yule aliyeandaliwa alienda kudai ujira wake kwa waliomwagiza, huku nyuma yeye alikuwa akitafutwa ili apigwe lakini alikimbia na kwenda polisi.
Anasema kama jambo hilo lingefanikiwa angerithiwa na ndugu wa mume wake.
Anasema kwa kufanya hivyo ndio maana wanawake wengi wa vijijini wanaambukizwa magonjwa mbalimbali.
Daktari wa Kituo cha Afya cha Katesh, David Laizer anasema ndoa za utotoni zinazosababishwa na wazazi ni ukatili mkubwa, kwa kuwa kitendo hicho si kwa ridhaa ya muolewaji.
Pia anasema ukatili mwingine anaouana ni ule wa kuwapeleka watoto wa kiume shuleni na kuwaacha wa kike. Huo ni ukatili uliopitiliza kwa jamii hiyo.
Pia wanaume kutelekeza wake zao na watoto ni ukatili mkubwa kwa kuwa watoto wale wanateseka kwa kukosa mahitaji muhimu.
Wengi wanatelekezwa ama kuachika wanakuwa hawana sehemu za kwenda hali inayoleta mateso kwa watoto.
Kwa upande wake Mtendaji wa Katesh, Peter Mando anasema katika eneo hilo ukatili wa kijinsia upo sana kwa wanaume kuwapiga wake zao pamoja na kuwafukuza nyumbani.
“Migogoro kama hii tunaisuluhisha sana sisi na maofisa wa jamii, mahakama na polisi. Bado changamoto hiyo ni kubwa sana,” anasema.
Anasema katika kutatua migogoro hiyo wanawatumia maofisa wa maendeleo ya jamii kusuluhisha ikiwa ni pamoja na wazee wa mila na mahakama.
Chanzo cha jambo hili anasema ni mila na desturi za huko kwani wanaume wamekuwa wakiwabeza sana wanawake, ugumu wa maisha kwani wanandoa wengi wamekuwa wakizozana kwa ajili ya mahitaji ya nyumbani.
Si hivyo tu, bali na unywaji wa pombe pamoja na kutokufanya kazi, ndiyo inaleta shida hii.
Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Katesh A, Petro Tehhan anasema ukatili wa kijinsia eneo hilo unasababishwa  na mfumo dume pale baba anataka kusema kila kitu.
Pia kutokuelewana kwa mume na mke kunasababisha hali hiyo.
Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Hanang Kituo cha Katesh, Hamis Mwampelwa anazungumzia kesi za ukatili wa kijinsia zilizoripotiwa kituoni hapo ni 161, kati ya mwaka 2014 hadi sasa.
Anasema katika kesi hizo zile zilizofungwa ambazo hazikufikishwa mahakamani ni kesi 38, zilizofikishwa mahakamani ni 59 na zilizo chini ya upelelezi ni 70.
Kati ya kesi hizo, Mwampelwa anasema zilizopata mafanikio ni 15, ambazo hazikupata mafanikio ni 14, kesi iliyopo mahakamani kwa mwaka huu ni moja.
Anaeleza miongoni mwa kesi zilizoripotiwa za unyanyasaji wa kijinsia kuwa ni zile za kutelekeza familia, kubaka, shambulio la aibu pamoja na ukatili dhidi ya mtoto.
Anatoa mfano kwa kesi moja iliyofikishwa kituoni hapo siku za karibuni.
Kesi hiyo inamhusu mkazi wa Kitongoji cha Qedang’onyi Emanuel Lambo (50), aliyetarajiwa kufikishwa mahakamani baada ya kumtendea vitendo vya ukatili mtoto wake wa miaka tisa wa shule ya msingi kwa kumchoma na kisu chenye moto mkali maeneo mbalimbali ya mwili.
Mwampelwa anasema mtoto huyo alichomwa moto maeneo mbalimbali ya  mwili, kwenye kiwiko mkono wa kulia, kwenye shavu kushoto, shingoni kushoto, usoni na sehemu mbalimbali za mguu upande wa kulia kutokana na kulala kwa kaka yake, Mussa Emmanuel.
Anasema Oktoba 15 sueta la shule la mtoto huyo lilikuwa halijakauka, mama yake akamwagiza kaka yake akamuombee ruhusa shuleni, kisha mtoto huyo akalala kwa kaka yake huyo ndio ilikuwa chanzo cha baba kutenda ukatili huo.
Anasema mwanafunzi huyo aliwaambia wakati akitendewa ukatili huo, mama yake alijitahidi kumwokoa lakini baba yake alimkataza.
Tukio hilo la mwanafunzi kutendewa ukatili, lilijulikana baada ya mwalimu wake Bahati Mwiru kuhakiki wanafunzi shuleni na kugundua mtoto huyo hayuko, ndipo wenzake wakamwambia ana majeraha.
“Mwalimu aliendelea kuuliza wanafunzi hao majeraha  ni ya nini, ndipo wakamwabia amechomwa moto na kisu. Wakaijulisha kamati ya shule, mwenyekiti na mlinzi wakaenda kumchukua nyumbani,” anasema.
Anasema mwalimu huyo alitoa taarifa polisi baada ya mtoto huyo kukosekana shuleni kwa muda na alipouliza wenzake walimwambia anatibu majeraha aliyosababishwana baba yake, ndipo wakaanza kumfuatilia.
mwisho

Ukeketaji Mbulu


 
Helena Ringo: Mimi ni mfano wa watu waliokeketwa
Joan Michael: Nilipokeketwa damu na usaha ilitiriria
DK.Leonard Tlatlaa: Nimekutana na mtoto njia ya uzazi imefunga kwa ajili ya kukeketwa
Na  Lucy Ngowi
“NAKUMBUKA nilipokuwa na miaka mitano nilikeketwa. Kiukweli sitaisahau siku hiyo kutokana na maumivu niliyoyapata wakati wa kukeketwa na kuuguza kidonda.
“Wakati naugulia maumivu ya kukeketwa, nilikuwa nikiona katika sehemu zangu za siri damu na usaha vikitiririka, ila sijui mbele ya safari itakuwaje, kama atakuwa na uwezo wa kupata mtoto au la,” anasema Joan Michael (jina lisilo rasmi).
Binti huyo ambaye hivi sasa ana miaka 19 anazungumza kwa uchungu kuelezea mila potofu zinazofanywa na kabila lake la wabarbaig.
Anasema laiti kama angechelewa kukeketwa asingekubali tena kwani katika hali ya uhalisia ni ukatili uliopitilizwa, kwani hata kwenye maandiko matakatifu biblia hakuna mahali inapozungumzia kuhusu kumkeketa mwanamke bali kutahiri wanaume.
Anaiomba Serikali kuendelea kutoa elimu bila kuchoka kwa jamii hiyo ili kuwanusuru watoto wa kike ambao bado hawajakeketwa wasipatwe mateso ambayo alikabiliana nayo.
Si huyo tu, mfano wa binti  kama huyo ni mingi katika jamii za watu wanaokeketa ila wamekuwa wakiogopa kuzungumza hadharani kwa kuona aibu au kuhofia kutengwa na ndugu zake.
Kwa upande wake Mama Mchungaji wa Kanisa la Evangelistic Assemblies of God (EAGT), Odeliana Emmanuel anasema katika kijiji cha Qandach alikozaliwa, kata ya Endamila wilaya ya Mbulu, amekuwa akiona hali ya ukeketaji kwa watoto wa kike.
Anasema kama mama mchungaji na mwanaharakati wa kumtetea mtoto wa kike, amekuwa akizungumza na wale wanaowaandaa watoto kuwapeleka kwa ngariba, kuwaelimisha na kuwafundisha athari za kukeketwa kwa mtoto wa kike.
“Nimeelimisha ubaya wa ukeketaji. Kwa sasa umepungua lakini unaendelea kwa siri sana, hivyo wamebadili mbinu mpya ya kuwakeketa watoto kuanzia wanapoanza kutembea,” anasema mwanaharakati huyo.
Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Mbulu, Halmashauri ya Vijijini Justino Bayo anasema wilaya hiyo ina wenyeji wanaojulikana kama wairaqw, datoga au barbaig, nyisanzo na hadzabe.
Anasema suala la ukeketaji katika wilaya hiyo sasa hivi linapungua kwa wairaqw pamoja na wanyisanzo, lakini wa wabarbaig wanaendelea.
Lakini kama tendo hilo linafanyika katika mji  huo  ni kwa siri sana kutokana na kuogopa mkono wa sheria.
Bayo anasema chanzo cha hilo ni mila na desturi za wenyeji ambao wanaona kuwa mwanamke asipokeketwa ni kama najisi.
Naye Helena Ringo anaeleza kuwa, yuko miongoni mwa waliokeketwa, kwani mbaya zaidi alifanyiwa kitendo hicho akiwa na miaka 19 baada ya kumaliza chuo.
“Mimi ni mfano wa watu waliokeketwa. Nilikeketwa nikiwa nimemaliza chuo cha ualimu nikiwa na miaka 19,” anasema.
Mwanamke huyo ambaye fani yake ni mwalimu pia ni Mratibu wa Shirika linaloshughulikia ukeketaji wanawake na wasichana (AFNET), anasema mara nyingi mwisho wa mwaka wanawake wengi wanaandaa wasichana wao kwa ajili ya kukeketwa.
Hivyo kama mwanaharakati amekukwa akipita shule mbalimbali na kuwaasa wanafunzi wasikubali kukeketwa kipindi cha likizo.
Anasema amekuwa akipita katika shule za msingi na kutoa elimu hiyo, si hivyo tu bali mara nyingi pale anapokuta watu wamekusanyika huomba nafasi na kusema machache kuhusu ubaya wa ukeketaji.
“Nimekuwa nikiwaambia msipunguze kiungo chochote cha mtoto katika mwili wake, endapo mtafanya hivyo akimkamata mtu yeyote anampeleka mahakamani,” anasema mwanaharakati huyo.
Si hivyo tu, bali hata siku ya mtoto wa Afrika inayofanyika Machi 16, huwa anatoa elimu hiyo kuhusu ukeketaji.
Anakiri kuwa tatizo hilo ni kubwa, hivyo kama wataendelea kutoa elimu litapungua.
Anaongeza kuwa, baada ya kutolewa elimu mara kwa mara kuhusu athari za ukeketaji tatizo linapungua isipokuwa kwa watu wa vijijini ambao hufanya kimya  kimya ili wasijulikane wanachokifanya.
Ringo anasema chanzo cha ukeketaji ni imani iliyojengeka kuwa wanawake wanakeketwa ili kupunguza uhuni, lakini kiuhalisia ndio waliozidi kwa tabia hiyo mbaya.
Sababu nyingine ni kwamba wanamfanyia usafi msichana huyo kwa sababu sehemu hiyo inaficha uchafu.
Naye Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya Mbulu, Dk. Leonard Tlatlaa anasema hawajapata kesi za mtu aliyezidiwa kutokana na kukeketwa lakini kama daktari anaona kuna dalili zinazoonyesha bado kuna ukeketaji.
Na kwamba katika eneo hilo wanakeketa watoto katika umri mdogo kwa kuogopa mkono wa sheria.
“Kama daktari nimekutana na kesi ya mama wa mtoto kusema mtoto wake hana njia ya uzazi, nilipomcheki nikagundua njia iko wazi na kuna kidonda kilichotokana na kukeketwa,” anasema.
Anaongeza kuwa kati ya mwaka jana na mwaka huu amekutana na wagonjwa watatu wenye matatizo yaliyosababishwa na kukeketwa. Anasisitiza ukeketaji uliopo hivi sasa unafanywa katika umri mdogo.
Akizungumzia athari za ukeketaji ni kupoteza damu nyingi,  pale anapokeketwa mtu kinatokea kidonda na kutengeneza usaha ambao hupandisha homa na kuleta ufinyu wa njia ya uzazi hivyo mama wakati wa kujifungua huchanika.
Anasisitiza katika wilaya hiyo ukeketaji upo kila mahali.
Chanzo chake ni mila na desturi kwa kuwa watu hawataki kubadilika , pia wanasema kama msichana hajakeketwa hafai kuolewa. Hiyo ni dhama potofu.
Anasema pamoja na elimu inayotolewa jamii bado haijakubaliana na hiyo dhana ya kutokukeketa kutokana na mila na desturi. Hiyo ni kasumba yao bado haijawatoka.
Anashauri elimu iendelee kutolewa kuhusu athari zake baadaye kuhusu uzazi bora.
Pia hata mkono wa sheria unapokuwepo ufuate mkondo wake.
Mratibu wa Shirika la Afya na Maendeleo (Gesodea) pia Mwenyekiti wa Mtandao wa Malezi, Makuzi na Maendeleo ya mtoto mdogo, Tawi la Manyara  Jackson Suloo anakiri ukeketaji Mbulu umepungua kutokana na elimu inayoendelea kutolewa.
Pia anaamini miaka ijayo tatizo hilo litakuwa limekwisha, na kwamba tokea mwaka jana hadi sasa taasisi yake imezungumza na wazazi 83 kuhusu athari za ukeketaji.
Anaelezea chanzo cha ukeketaji ni kwamba ngariba wanatafuta kipato.
Kwa upande wake WP 4728 Koplo Glory kutoka kituo cha Polisi Mbulu anayeshughulikia dawati la jinsia anasema, kituoni hapo hakuna kesi zozote za ukeketaji zilizofikishwa.
Wilaya ya Mbulu ni mojawapo ya wilaya zilizopo katika Mkoa wa Manyara. Katika sensa ya mwaka 2012 idadi ya wakazi wa wilaya hiyo ilihesabiwa kuwa 320,279 waishio humo.
Mbulu imepakana na Mkoa wa Arusha pamoja na ziwa Eyasi upande wa kaskazini, wilaya ya Babati Vijijini upande wa mashariki, wilaya ya Hanang upande wa kusini na mkoa wa Singida kwa magharibi.
Wenyeji asilia ni Wairaqw  ama wanajulikana kama Wambulu. Makao makuu yapo Mbulu mjini na mji huu ulianzishwa wakati wa koloni ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani kwa jina la Neu-Trier.
Ukeketaji hapa nchini badi upo katika baadhi ya  maeneo kama mkoa wa Manyara, Dodoma, Arusha, Singida, Mara, Kilimanjaro na Morogoro.
Kati ya mikoa hiyo saba, Mkoa wa Manyara ndio unaongoza kwa asilimia 70.8 na Morogoro ndio wa mwisho kwa asilimia 21.1.

Ndoa za utotoni


Na Lucy Ngowi
NDOA za utotoni huathiri afya kwa kuwa mwili wa mtoto unakuwa hauko tayari kukabiliana hali hiyo, pia huleta athari za kisaikolojia.
Katika Wilaya ya Hanang, Mkoani Manyara kuna tatizo la kuwepo kwa ndoa za utotoni hali inayosababisha wasichana kupata mimba katika umri mdogo.
Inaelezwa kuwa katika wilaya hiyo ndoa za utotoni zipo lakini sio kama ilivyokuwa zamani, na kwamba watoto wanavyoolewa sio hiari yao bali hulazimishwa na wazazi wao.
Hapo zamani kwa kabila la wabarbaig msichana alikuwa haruhusiwi kuzungumza lolote kuhusu kijana anayempenda, ila wazazi ndio walikuwa wakiwatafutia wachumba.
Ama msichana anapokuwa akichunga kijana anayempenda humkamata na kuishi naye, kwa siku chache endapo msichana atarudi nyumbani kwao, wazazi wa binti huyo humrudisha kwa kijana huyo.
Mwanamke Anna Mussa (jina lisilo rasmi), anasema alipewa mimba akiwa na miaka 12, hivi sasa ana watoto watano.
Anasema akiwa katika hali hiyo  mwanzoni haikuwa rahisi kwa kuwa hakuweza kumudu maisha ya ndoa, lakini kwa kuwa mwanamme huyo aliamua kuishi naye hivi sasa wana watoto hao watano.
Kwa maelezo yake alizaliwa mwaka 1979, hivi sasa ana watoto wakubwa kabisa ambao wengine wameolewa na kuoa na wengine bado wapo shuleni.
“Kwangu mimi niliona kama nimepata bahati kwa kuwa vijana wengi wanawapa wasichana wadogo mimba kasha huwakimbia, hawako tayari kuwahudumia kwa jambo lolote lile. Huyu wa kwangu alikubali tuendelee kuishi hadi hivi leo,” anasema mwanamke huyo.
Akizungumzia hilo Ofisa Maendeleo ya Jamii wilaya ya Hanang, Sabina Sulle anasema ndoa za utotoni zinaenda sambamba na mimba za utotoni.
Watoto wengi wanaopata mimba hufika ofisini kwao kwa ajili ya kulalamikia kutopata matunzo ya watoto au mtoto aliyezaliwa.
Anasema kesi za utelekezaji wa watoto ofisini kwao zipo nyingi, ambazo hupelekwa hapo kwa ajili ya kutafuta ufumbuzi wa jinsi ya kumlea mtoto au watoto waliozaliwa.
Anasema ofisini kwao, wana kesi ya binti moja mwenye miaka 17 ambaye alipata mimba utotoni.
“Binti huyo alizaa na mume wa mtu, hivyo akawa hapati matunzo baada ya kujifungua. Kesi ilipofika kwetu tukaitatua kwa kumwamuru mwanamme huyo kumtunza mtoto hadi atakapofikia miaka 18,” anasema.
Pia ushauri mwingine wanautoa wanashauri mtoto atakapofika miaka 17 anatakiwa kuulizwa kama anataka kuishi na baba yake.
Anasema kesi nyingine walizonazo ni za kutekeleza watoto. Hizo zipo nyingi kwa kuwa wanaume wengi hawawatunzi watoto hivyo pale wanawake wanapozidiwa huenda ofisini kwao kutafuta msaada.
Pamoja na kutatua kesi nyingi, ofisa huyo anasema kuna changamoto zake kwani wanaume wengi ni waongo wanaweza kuzungumza kuwa watawatunza watoto baada ya kufikishwa hapo lakini utekelezaji unakuwa haupo.
“Hivi sasa tuna daftari mtu akija kushtakiwa anatakiwa alete hela hapa ofisini  na huyo mwanamke aifuate hapo. Mwanamme anapopeleka hela anasaini na mwanamke anapochukua pia,” anasema na kuongeza kuwa kesi hizo zinazidi 30.

JINSI YA KUPANGILIA MALENGO YAKO NA LUCY NGOWI




JINSI YA KUPANGILIA MALENGO YAKO

SOMAJI wangu, nakukaribisha tena katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, zinzokujia kila Alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi unavyoweza kupanga malengo makubwa katika maisha yako.
Watu wengi hushindwa kufikia malengo makubwa kwa kuwa, mara zote hujikatisha tamaa kuwa hawawezi kufanya jambo kubwa la kimaendeleo, kabla ya kujaribu kulifanya.
Tabia ya baadhi ya watu hao wanaokuwa na malengo madogo katika mazingira wanayoishi, ina maanisha eneo hilo hakuna ushindani wa kimaendeleo, ama wao wenyewe hawana jitihada za dhati za kupiga hatua zaidi mbele.
Lakini ikimbukwe kuwa, katika kutafuta mafanikio hayo ili uwe na maisha bora, usimwangalie mtu jinsi alivyo, kwamba ana urefu gani, ana pesa kiasi gani, digrii aliyonayo ama kuangalia historia ya maisha yake, bali hupimwa kwa uwezo wa kufikiri kwake.
Watu wengi wanaofikiria kuwa na malengo makubwa ya mafanikio, katika maisha yao ni kutokana na matarajio waliyonayo.
Inakupasa kila mara ujitahidi kupanua mawazo yako na kubuni mbinu mpya za kukutoa hapo ulipo na kukuweka katika hatua nyingine nzuri zaidi kimaendeleo.
Hivyo utambue kuwa, unapotaka kufanya mambo makubwa inakupasa ujijue wewe ni nani na una thamani gani.
Kwa maelezo mengine usijishushe hadhi yako kwa kuona kuwa huwezi kufanya mambo makubwa ya kimaendeleo ambayo yatakutoa hapo ulipo na kukuweka katika hatua nyingine nzuri zaidi.
Tuangalie mfano wa kijana mmoja aliyeshindwa kupiga hatua mbele baada ya kujishusha hadhi yake na kujiona hawezi.
Kijana huyo, aliona tangazo la kazi katika gazeti. Kazi aliyokuwa anapenda kuifanya na pia ameisomea.
Lakini hakufanya jitihada za dhati za kuomba nafasi ile, kwa kuwa alijiona hawezi kuipata hata kama angeomba.
Aliona kuliko ajitaabishe ni heri aache kuomba nafasi hiyo. Mfano huo si mzuri kwa mtu anayetaka kupiga hatua kimaisha.
Usijishushe hadhi yako ama usikatishwe tamaa kwa hali yoyote ile. Ni vema kujaribu kile unachokipenda na unachokihitaji katika maisha yako, kuliko kuacha kujaribu kwa kuogopa kuwa hautafanikiwa.
Kwani matokeo huja baadaye, hata utakaposhindwa, utakuwa na nguvu ya kujaribu tena sehemu nyingine.
Wengi wetu, tumekuwa tukijikatisha tamaa katika shughuli mbalimbali tuzifanyazo ama tunazotaka kuzifanya.
Yawezekana umeanzisha biashara kwa lengo la kukuinua kiuchumi, lakini matokeo yake, biashara hiyo haiendi kama vile ulivyotarajia.
Jambo la msingi, inakupasa kukaa chini na kujitathmini, kuangalia ni sehemu gani unayokosea.
Ama kuangalia, kama una washindani wengi katika eneo hilo, ili uweze kufanya vizuri zaidi yao, kwa kuweka vitu vingi tofauti na kuboresha eneo la biashara yako.
Kuwa mbunifu katika biashara yako kutakupa wateja wengi, na utafanikiwa zaidi. Cha msingi usikate tamaa katika kufikia malengo unayoyakusudia.
Kutokana na hali ya kujikatisha tamaa, miongoni mwa watu wengi, wanasaikolojia mbalimbali wamekuwa wakishauri ni vema, watu wajijue vile walivyo ili waweze kujirekebisha pale penye upungufu na kusonga mbele kimaisha.
Hali ya kujikatisha tamaa ni mbaya sana, ni sawa na ugonjwa usiopona katika mwili wako. Ili kuutibu ugonjwa huo, inakupasa ujielewe wewe ni nani, na una upungufu gani, pamoja na kukubali mabadiliko.
Tatizo kubwa lililopo kwa watu wengi, hawajui kuwa, wao wana uwezo mkubwa tofauti na wanavyojifikiria.
Hivyo ni vema kuweka mawazo yako kwenye kipimo halisi, uyachuje na kuchukua yale yaliyo na thamani.
Penda kufikiri mambo makubwa. Usijishushe hadhi yako kwa kujiwekea au kufikiri malengo madogo. Anza sasa kuwaza mambo makubwa ili uwe mtu mwenye ndoto njema ya maendeleo.
Kutokana na hali hiyo ya watu kujikatisha tamaa, wale ambao wamewahi kufanya biashara na kufilisika, wengi wao wamekuwa wakisema kuwa hawatarudia tena kufanya biashara hiyo.
Lakini kumbe, haikuwapasa kukata tamaa, bali kujipa moyo, na kuelewa kuwa pamoja na hali hiyo ya kushindwa inawapasa kujaribu tena.
Kamwe usikate tamaa katika jambo lolote unaloliwaza ama kulifanya. Kwa kuwa, upo msemo mmoja unaosema, penye nia pana njia.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’, kilichotungwa na David Schwartz pamoja na mitandao mbalimbali.

Kwa maoni, ushauri wasiliana nasi nami kwa

simu 0713 331455; 0767331455


FAHAMU KANUNU ZA KUISHI VIZURI na LUCY NGOWI lucyngowi2009@gmail.com



FAHAMU KANUNU ZA KUISHI VIZURI

 na LUCY NGOWI      

 lucyngowi2009@gmail.com




KARIBUNI tena wapenzi wasomaji wa safu hii ya kila Alhamisi. Wiki iliyopita tulizungumzia kuhusu kuepuka tabia ya ukali, ukaidi na ugomvi. Leo tutaona kanuni au mbinu nyingine za kuishi na watu vizuri, ukiwa ni mwendelezo wa pale ilipoishia.

Epukana na biashara au na shughuli zisizo halali. Unapofanya shughuli au biashara isiyo halali inakuondolea uaminifu kwa jamii inayokuzunguka.
Kwa mfano, kama mtaani au kazini kwako unakuwa mtu usiyeeleweka kwa kuwa watu wanajiulizauliza kile unachofanya na wasipate majibu, hiyo si jinsi au njia nzuri ya kuishi na watu.
Vile vile biashara hizo zinaweza kukusababishia matatizo kama ya kufunguliwa mashitaka na kufikishwa mahakamani endapo utakutwa na kosa.
Jifunze kutokuwa mchoyo au uwatakie watu wengine mambo mema. Baadhi ya watu waliofanikiwa huwa hawapendi maendeleo ya wengine. Wanapoombwa msaada ni wagumu kutoa.
Mfano kwa baadhi ya wanafunzi shuleni wakiojaaliwa kuwa na uwezo kiakili huwa hawapendi kutoa msaada kwa wenzao. Hata maofisini kuna baadhi ya watu wasiopendi maendeleo ya wenzao kwa kumsemea mambo yasiyo ya kweli kwa bosi wao.
Epukana na lugha ya ubinafsi, mfano: mimi, changu, n.k. Badala yake tumia chetu, sisi n.k. Lugha hizo si nzuri katikati ya jamii inayokuzunguka. Unapokuwa na tabia hiyo inakujengea chuki miongoni mwa wanaokuzunguka. Ni vizuri kushirikiana vifaa vya ofisini, shuleni na katika maeneo mbalimbali na jamii.
Inawezekana wakati mwingine mtu anakuwa na lugha hiyo ya ubinafsi kutokana na mazingira yaliyopo. Mfano wewe ni msafi na wenzake unaoishi nao, kufanya kazi nao au kusoma nao wanakuwa na tabia ya uchafu. Kama umeshajaribu kuwabadilisha bila mafanikio, ni vizuri kutumia busara ya kununua vitu kama vyako na kuwapa vile ambavyo una uwezo navyo.
Hii itakusaidia kila mtu kutumia kifaa chake, mfano vikombe maofisini - kila mtu ana usafi wake, vioo kwa akina dada, chanuo za kuchania nywele na mfano wa vitu kama hivyo. Jitahidi kutokuonyesha hali hiyo kwa gharama yoyote ile.

Thamini utu wa mtu bila kujali uwezo au nafasi yake katika jamii. Kumbuka kwamba siku hazifanani, kwani waweza kupokea msaada mkubwa wa kimawazo au wa hali kutoka kwa mtu usiyemtarajia.
Watu wengine wanapotoa msaada kwa wenzao hujisahau na kuanza kutangaza au kumnyanyapaa yule aliyemsaidia huku akiona ni sawa.
Mfano rahisi unakuta labda kuna watu wengine wamewapokea ndugu zao au watu ambao hawana uwezo na kuishi nao nyumbani kwao. Kutokana na kuishi naye basi ufadhili unageuka kuwa mateso kwa kuwa kila kazi ataifanya huyo aliyesaidiwa au kila mara atakuwa anatumwa maeneo ya mbali mara nyingine pasipo hata na nauli.

Si vibaya kumtuma wala si vibaya kusaidiwa na mtu kama huyo, ila isivuke mipaka kwani itakujengea picha mbaya kwa wanaokufahamu pamoja na huyo unayemsaidia atakapoamua kuondoka kwako.
Epukana na tabia ya kugombeza, kutukana au kudharau wengine. Iwapo watu walio chini yako wamekosea au wamefanya kinyume na ulivyotarajia; jaribu kuwaelekeza kwa upole bila kutumia jazba au hasira. Usiendekeze lugha za matusi, dharau au ugomvi, kwani huweza kushusha hadhi yako na hata utu wako.
Watu wengine wamejiendekeza katika tabia ya kupenda kugombagomba ovyo hata bila sababu, wengine hudiriki hata kutukana au kudharau wengine.

Hii ipo sana maofisini. Mabosi walio wengi hujisahau kuwa nafasi wanazokalia ni za muda tu, hivyo hudharau wale walio chini yao kwa kuwasemasema ovyo na kuwatukana pasipo sababu ya msingi.
Hata kwa upande wa baadhi ya wanawake na wanaume wawapo nyumbani kwao huwa na tabia hiyo kwa watoto wao, wafanyakazi waliowaajiri au ndugu wanaoishi nao.

Ni vizuri kuacha tabia hiyo, kwani inakuondolea heshima na kukufanya udharaulike.
Pia wakati mwingine utakuta wenye mali si wasemaji, lakini wale wanaowaachia majukumu kidogo ndiyo wanaokuwa na tabia hizo mbaya katika jamii. Gombeza pale inapostahili lakini isiwe mazoea, kamwe usitukane wala kuleta dharau kwa wengine. Huo ni utovu wa nidhamu.

Jifunze kuvumilia mienendo ya imani ya dini nyingine. Watu wengine wana tabia ya kudharau au kutothamini misimamo ya wengine ya kiimani. Utamkuta mtu anakashifu hadharani dini za watu wengine kwa kutumia vigezo visivyokuwa na maana.
Suala hili katika jamii yetu inayotuzunguka limekuwa likileta mizozano na wakati mwingine watu huamua kupigana. Mnapokuwa watu wenye imani za dini tofauti katika ofisi zenu, vyuoni au hata kwenye mikusanyiko mbalimbali, jaribu kuvumilia kila hatua ambayo kwako unaiona ni kinyume na maadili yako. Ukishindwa hali hiyo ni vizuri uondoke na kuwapisha wenyewe waendelee.

Kwa mfano, kwenye msiba labda wewe ni wa madhehebu fulani, hivyo umekwenda kwenye msiba wa imani tofauti na yako, ni vizuri kufuata taratibu zilizopo mahali pale, na kama unajiona huwezi basi ili kuepusha shari ondoka eneo hilo uwaachie wenyewe ili usionekane ni kituko.

Ni vizuri ukae kimya uwaachie wenyewe waendelee na ratiba na shughuli zao kuliko kuanza kupayuka ovyo au kukosoa katika msiba huo. Tulia wakimaliza shiriki nao kwenye msiba ndivyo maisha yalivyo.
Usiwe mkali kwa watu, jenga uhusiano mzuri. Ukali ni hulka ambayo huwafanya watu wawe mbali na wewe na hata kusababisha kukosa marafiki. Unaweza kukuta mtu ana nafasi nzuri katika jamii lakini hakuna mtu mwenye mazoea naye kutokana na ukali wake. Mfano katika ofisi mwajiri unakuwa mkali kiasi kwamba wafanyakazi wako wanakosa uhuru wa kujieleza kwako wanapokuwa na matatizo yao binafsi au ya kiofisi.
Unapokuwa na uhusiano mzuri na watu; hali hiyo inakufanya kukubalika, kuheshimika, kupendwa na jamii inayokuzunguka. Mfano mwalimu anapokuwa karibu na wanafunzi wake, huweza kuvuta hisia zao za usikivu na hatimaye kufanya vema katika masomo yao.

Uwe mwangalifu sana na mwanamke/mwanaume asiyekuwa wako. Siku zote mazoea na watu wa jinsia tofauti na ya kwako lazima yawe na mipaka. Kuna watu ambao hawawezi kutawala hisia zao hata wanapokuwa na wenzao ambao tayari wana familia zao.
Hii inajitokeza sana shuleni, vyuoni, maofisini na hata maeneo ya kuishi; unakokuta msichana au kijana anakuwa na mazoea yaliyopitiliza na mume au mke wa mtu, hali inayoweza kusababisha mtafaruku kati ya pande husika.
Wakati mwingine unakuta wanawake/wanaume waliooa au kuolewa wanakuwa na mahusiano ya kimapenzi nje ya ndoa zao, hali inayosababisha kutoelewana baina yao na wenzi wao; wakati mwingine hata kusababisha kuvunja ndoa zao.


Kwa maoni, ushauri wasiliana nasi nami kwa

simu 0713 331455; 0767331455






ACHA MAWAZO FINYU


KATIKA makala zangu za Maisha Yetu niliwahi kuandika kwamba njia pekee ya kufanikiwa ni kutoruhusu mawazo yanayoleta kizuizi, kama vile kuwaza umaskini, kuwa na hofu au wasiwasi kila mara kwa kile unachokifanya.
Endapo wewe ni mtu wa aina hiyo inakupasa ubadilike ili usonge mbele kimafanikio.
Mara tu unapomaliza kuyachuja mawazo yako, unachagua yale unayotaka kuyafanyia kazi. Utagundua kuwa nayo yanahitaji kuongezewa ubora wake. Jifunze kutokufunga milango yako ya kuwa mbunifu.


Ni jambo lisilowezekana kati yetu kuwa kinyume cha ujuzi tulionao.
Mfano mtu hawezi kupita mbele ya gari liendalo kasi kwa kuwa anajua kuwa ataumia, hawezi kuogelea baharini kama anajua atazama, hawezi kuwa mstari wa mbele katika jambo la hatari kama anajua kuwa atadhurika.
Mafanikio hayahitaji kuwa na kiasi kikubwa cha ujuzi juu ya jambo fulani, lakini unatakiwa kung’ang’ania ili uweze kupata mafanikio hayo kwa ujuzi wowote ulionao.
Mkulima mmoja aliyejulikana kwa jina la Walter na ambaye siku za usoni angependa kuwa mchezaji bora wa mpira wa miguu, alimuuliza rafiki yake kuwa amewezaje kupata sh milioni 10 katika kazi yake anayoifanya kutokana na ujuzi alionao na kuweza kushinda kila dhana ya kushindwa ambayo ilikuwa inaibuka katika utendaji wake?
Rafiki huyo alimjibu kuwa wakati anaanza, alijua anataka kufanya nini na anachotarajia kukipata.


Alikuwa na njozi iliyomwezesha kujenga picha katika mawazo yake kulingana na malengo aliyotaka kuyafikia katika maisha yake.
Hivyo hiyo ndiyo siri kubwa ya mafanikio katika maisha yake.
Walter anasema kuna wakati alisikia umati wa watu ukishangilia katika mawazo yake.
Kuna wakati alijenga picha ya sherehe ya kupewa tuzo iliyojaa waandishi wa habari za michezo, wageni na wanamitindo mbalimbali.
Ndoto hiyo sasa ameanza kuifanyia kazi, hivyo anaamini atafanikiwa kama rafiki yake huyo alivyofanikiwa.


Inaonesha watu wengi wamekuwa hawako tayari kutulia na kufanyia kazi ndoto zile wanazokuwa nazo, kwa kuzipa nafasi ndogo katika utekelezaji wake.
Kuna mamilioni ya watu wanaoamini wanaangamia kwa umaskini na kushindwa kwa sababu baadhi ya malengo waliyonayo wamekuwa hawawezi kuyafanyia kazi.
Bila kujua watu wengi hujitengenezea mazingira mabaya kutokana na mawazo hasi yanayochukuliwa na mawazo na kutafsiriwa kwenda katika vitendo.
Kwa sasa hivi utaweza kutambua kwamba mawazo ni vitu ambavyo kama vikifanyiwa kazi vizuri na kutekelezwa vinaweza kuwekwa katika mfumo wa uhalisia.
Kama utakuwa na njozi za kupata zaidi na ukazijengea picha hiyo bila kujali utakumbana na vikwazo gani, hiyo itakuwa ni vipaumbele katika maisha yako.
Kama utaruhusu picha ya namna hii kuwa ya kudumu katika ulimwengu wako wa mawazo; utafikiri mawazo ya mafanikio na kuzungukwa na watu wenye mafanikio watakaotia moyo njozi zako.

Utatenga sehemu ya kipato chako kwa ajili ya kujilipa wewe mwenyewe, moja ya hatua muhimu katika kupata utajiri.
Utajihusisha katika mpango unaoleta mafanikio binafsi na kukufanya uchague lengo la maisha yako.
Pia utatafuta ujuzi na utaalamu kwa wale wote ambao wamefanikiwa. Mwishoni utafanikiwa licha ya kukumbana na vikwazo katika kutekeleza njozi zako.


Kwa maoni, ushauri wasiliana nasi nami kwa

simu 0713 331455; 0767331455



ACHA MAWAZO FINYU NA LUCY NGOWI




ACHA MAWAZO FINYU


KATIKA makala zangu za Maisha Yetu niliwahi kuandika kwamba njia pekee ya kufanikiwa ni kutoruhusu mawazo yanayoleta kizuizi, kama vile kuwaza umaskini, kuwa na hofu au wasiwasi kila mara kwa kile unachokifanya.
Endapo wewe ni mtu wa aina hiyo inakupasa ubadilike ili usonge mbele kimafanikio.
Mara tu unapomaliza kuyachuja mawazo yako, unachagua yale unayotaka kuyafanyia kazi. Utagundua kuwa nayo yanahitaji kuongezewa ubora wake. Jifunze kutokufunga milango yako ya kuwa mbunifu.


Ni jambo lisilowezekana kati yetu kuwa kinyume cha ujuzi tulionao.
Mfano mtu hawezi kupita mbele ya gari liendalo kasi kwa kuwa anajua kuwa ataumia, hawezi kuogelea baharini kama anajua atazama, hawezi kuwa mstari wa mbele katika jambo la hatari kama anajua kuwa atadhurika.
Mafanikio hayahitaji kuwa na kiasi kikubwa cha ujuzi juu ya jambo fulani, lakini unatakiwa kung’ang’ania ili uweze kupata mafanikio hayo kwa ujuzi wowote ulionao.
Mkulima mmoja aliyejulikana kwa jina la Walter na ambaye siku za usoni angependa kuwa mchezaji bora wa mpira wa miguu, alimuuliza rafiki yake kuwa amewezaje kupata sh milioni 10 katika kazi yake anayoifanya kutokana na ujuzi alionao na kuweza kushinda kila dhana ya kushindwa ambayo ilikuwa inaibuka katika utendaji wake?
Rafiki huyo alimjibu kuwa wakati anaanza, alijua anataka kufanya nini na anachotarajia kukipata.


Alikuwa na njozi iliyomwezesha kujenga picha katika mawazo yake kulingana na malengo aliyotaka kuyafikia katika maisha yake.
Hivyo hiyo ndiyo siri kubwa ya mafanikio katika maisha yake.
Walter anasema kuna wakati alisikia umati wa watu ukishangilia katika mawazo yake.
Kuna wakati alijenga picha ya sherehe ya kupewa tuzo iliyojaa waandishi wa habari za michezo, wageni na wanamitindo mbalimbali.
Ndoto hiyo sasa ameanza kuifanyia kazi, hivyo anaamini atafanikiwa kama rafiki yake huyo alivyofanikiwa.


Inaonesha watu wengi wamekuwa hawako tayari kutulia na kufanyia kazi ndoto zile wanazokuwa nazo, kwa kuzipa nafasi ndogo katika utekelezaji wake.
Kuna mamilioni ya watu wanaoamini wanaangamia kwa umaskini na kushindwa kwa sababu baadhi ya malengo waliyonayo wamekuwa hawawezi kuyafanyia kazi.
Bila kujua watu wengi hujitengenezea mazingira mabaya kutokana na mawazo hasi yanayochukuliwa na mawazo na kutafsiriwa kwenda katika vitendo.
Kwa sasa hivi utaweza kutambua kwamba mawazo ni vitu ambavyo kama vikifanyiwa kazi vizuri na kutekelezwa vinaweza kuwekwa katika mfumo wa uhalisia.
Kama utakuwa na njozi za kupata zaidi na ukazijengea picha hiyo bila kujali utakumbana na vikwazo gani, hiyo itakuwa ni vipaumbele katika maisha yako.
Kama utaruhusu picha ya namna hii kuwa ya kudumu katika ulimwengu wako wa mawazo; utafikiri mawazo ya mafanikio na kuzungukwa na watu wenye mafanikio watakaotia moyo njozi zako.

Utatenga sehemu ya kipato chako kwa ajili ya kujilipa wewe mwenyewe, moja ya hatua muhimu katika kupata utajiri.
Utajihusisha katika mpango unaoleta mafanikio binafsi na kukufanya uchague lengo la maisha yako.
Pia utatafuta ujuzi na utaalamu kwa wale wote ambao wamefanikiwa. Mwishoni utafanikiwa licha ya kukumbana na vikwazo katika kutekeleza njozi zako.